Jumanne, 11 Septemba 2018

KITABU: HUDUMA, KARAMA NA VIPAWA







ROHO MTAKATIFU KATIKA MAOMBI:
Huduma, Karama na Vipawa
.Na Shemasi Ismael Salehe











ROHO MTAKATIFU NA MAOMBI







Mwandishi:

Shemasi Ismael Salehe
  
  








Mhariri Johnson Pokeaeli
Mawasiliano: simu. +255782317895 +255754480661
                                   +255752513159+255654012268
NB: Hizi ni sura Nne tu; sura ya Tisa hadi ya Kumi na mbili wasiliana nasi kwaajili ya kupata kitabu kizima namba hizo hapo juu.
Ili kupata kitabu hicho itahitaji uchangie kidogo ili kuwezesha  kazi hii.
MUNGU AKUBARIKI!!
ROHO MTAKATIFU NA MAOMBI

Hatimiliki

Kitabu hiki ni mali halali ya Shemasi Ismael Salehe. Huruhusiwi kutoa nakala, hadi upate idhini kutoka kwa wachapishaji au kwa mwandishi wa Kitabu hiki.

©2016 Shemasi Ismael Salehe



























SHUKRANI


Namshukuru Mungu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu kwa kuniwezesha kufanya kazi hii. Pia nawashukuru wote waliohusika katika kufanikisha uandaaji na uchapishaji wa kitabu hiki. Kwa kipekee napenda niwashukuru hawa wafuatao:
Familia yangu: wamekuwa wavumilivu wakati wa mahangaiko ya kuandaa kitabu hiki, pia kwa ushauri waona maombi.
Mtheologia Johnson P. Pokeaeli: kwa ukaribu wake kwangu, ushauri, muda na marekebisho ya kazi hii. Pia amehusikakatika uchangiaji wa mawazo ya kuhakikisha kazi hii inafanikiwa. Ndiye aliyetengeneza kava la mbele na la nyuma la kitabu hiki.
Mtheologia Yohana E. Kakoa, kwa kushirikiana na Mtheologia Johnson katika marekebisho ya Kazi hii.
Mtheologia Mary Charamila, Kwa mchango wake wa mawazo na maombi. Amekuwa mshauri wa karibu kufanikisha kazi hii.
Jestina Mhando,kwa ushauri, mapendekezo, maombi na kutia moyo mpaka kukamilika kwa kazi hii.
Profesa Bagandashwa,kwa kuchangia, kushauri na kutoa marekebisho ya pendekezo la kitabu hiki. Na kipekee kwa msaada wake wa kifedha kwaajili ya kuchapishwa kwa kitabu hiki.
Daktari, Idahya, kwa kuchangia kushauri na kutoa marekebisho kwenye pendekezo la kitabu hiki. Amekuwa mtu wa karibu sana na mwenye utayari wa kunitia moyo wakati wowote na kunisaidia kimawazo pale nilipohitaji.
Daktari, M.Mbilu, Kwa kukubali kupitia na kkutoa marekebisho kwenye mapendekezo ya awali ya Kitabu hiki.
Daktari, E. Ngugi, Kwa kukubali kupitia na ndiye aliyeandika utangulizi wa kitabu hiki
Mch. Alice Kopwe, kwa mwaliko wake katika mkutano wa Paska wa wanafunzi wa Sekondari na vyuo, uliofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Ualimu Korogwe. Kwa mwaliko huo nilifanikiwa kuandaa somo hili.
Watheologia wenzangu katika chuo cha SEKOMU. Kwa kunitia moyo na kuchangia baadhi ya marekebisho katika kitabu hiki.
Mungu awabariki wote wallioshiriki katika maandalizi na uchapishaji wa Kitabu hiki.

















MATAZAMIO YA MWANDISHI WA ANDIKO HILI KWA MSOMAJI
Naamini andiko hili litakuwa jibu katika maswali ya watu wengi wanao jiuliza kuhusu maombi. Wakristo wengi wameshindwa kujua ni kwa nini hawapati majibu ya maombi yao. Wamefikia hatua ya kukata tamaa na kurudi nyuma katika Imani zao. Wanaomba lakini hawajibiwi. Wengine wanajiuliza ni kwa nini katika maombi wengine wananena kwa Lugha (Kuomba katika Roho Mtakatifu) lakini wao hawawezi? Pia kuna maswali mengi kuhusu hatua za kufuata mtu awapo katika maombi? au Ni faida gani mtu anayopata anapoomba katika Roho Mtakatifu? au Je! kuna kanuni za kuomba katika Roho Mtakatifu? au Ni jinsi gani mtu anaweza kujazwa Roho Mtakatifu? Je ni lazima kila Mkristo awe na ujazo wa Roho Mtakatifu? Na kuna hasara gani za Mkristo asipokuwa na Roho Mtakatifu?  Na jambo kubwa lililopo katika dunia ya sasa ni Mkristo kukubalika kwa muda mchache na badae kutokukubalika. Linalopelekea watu wengi kuwa na maswali mengi kuhusiana na kukubalika au kutokukubalika (Kuwa na kibali) mbele za wanadamu na mbele za Mungu. Kuna wanao jiuliza; Ni kwanini Mtu (mfanyakazi, au Mtumishi nk.) anakuwa na kibali kwa muda mfupi tu na baadae kimepotea, mfano anakuwa na mali badae zinaisha au anakuwa na anakuwa na wafuasi, marafiki wengi lakini baada ya muda wanamwacha. Yote haya na mengine mengi tutayapata katika mafundisho haya.
MUNGU AKUBARIKI.   AMEN.













YALIYOMO















SURA YA TISA

UMOJA WA KANISA


Waswahili wanasema Umoja ni nguvu utengano ni udhaifu” umoja ni mshikamano, makubaliano na mapatano ya kundi la watu. Ni mshikamano wa watu wenye nia na kusudi moja. Ni kufanya kwa pamoja mambo bila kutengana. “Kwa watu wengi umoja wa Kanisa ni maamuzi ya wakristo kuujenga mwili wa Kristo kwa vipawa mbalimbali. Hata hivyo tafsiri hii ya umoja wa kanisa, imekuwa ikikosewa na watu wengine, kwamba haijumuishi uhusiano wa kanisa na Mungu kinagaubaga. Kwa  watu kama hawa umoja wa kanisa pia unajumuisha wakristo na kanisa kwa upande wa Mungu na pamoja  na Mungu katika matendo na dhamira.”(Bagandashwa, 2016)
Mwito wa Mungu
Hili neno mwito linatumika kwa maana ya kupokea wajibu wa kumtumikia Mungu. Katika wajibu wa kumtumikia Mungu tunalazimika kuwa na mienendo na tabia zinazompendeza Mungu kama Neno la Mungu linanyosisitiza kwamba, “mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa, mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu, mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha.” (Kol 1:10_11) Tunahitajika kuzaa matunda ya imani yetu. Tukizaa matunda tutapata maarifa kutoka kwa Mungu. Mwito wa Mungu unafuatana na uwezo na mamlaka ya Mungu tukiwa na uvumilivu na kusubiri ahadi za Mungu. Tunapata furaha ya kudumu wakati tunapomtumikia Mungu. Hebu tuone andiko hili la Biblia linavyosema kwamba,“Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima naya ufunuo katika kumjua yeye.Macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilvyo na utajiriwa utukufu wa wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo. Na ubora wa uweza wakendani yetu tuaminio jinsi ulivyo, kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake.” (Efe 1:17_19)
Katika kumfuata na kumtumikia Mungu hakuna kunia makuu, kufuata Mungu kunaambatana na kuwa na kiasi. Mungu kama apendavyo amemgawia kila mtu kiasi cha imani “Kwa hiyo nawasihi, mimi niliyemfungwa katika Bwana, mwenende kama ilivyoustahili wito wenu mlioitiwa, kwa unyenyekevu na upole na uvumilivu, mkichukuliana na katika upendo ‘(Efe 4:1-2)
Wito wa kweli unatokana na Mungu Baba wa utukufu. Aliyeitwa na Mungu amepewa roho ya hekima. Mungu huwapa watumishi wake roho ya Ufunuo ili waweze kumjua Mungu wa kweli. Ili tufahamu kwa wazi tumaini letu lazima macho yetu ya ndani yatiwe nuru. Katika kumtumikia Mungu, tunapata utajiri wa urithi wake. Utendaji wa nguvu za uwezo wake unadhihirisha mamlaka tunayopata katika wito wa kumtumikia Mungu wetu. Wote wanaomtumikia ni mwili mmoja katika Roho mmoja. Walioitwa na Mungu wanasaidiana na kusameheana 1The 2:12.
Mtume Paulo anasema, “Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu kwa kuwa yeye amtumikiaye Kristo katika mambo hayo humpendeza Mungu, tena hukubaliwa na wanadamu.” (Rum 14:17_18)
Ufalme wa Mungu ni haki amani na furaha katika Roho Mtakatifu. Katika ushirika wa Roho Mtakatifu ni muhimu kujengana, Watu wa Mungu ni hekalu la Mungu wakishirikiana ni ushirika wa watakatifu. Roho Mtakatifu anakaa ndani ya hekalu ambalo ndiyo sisi. Tuthibishe katika Neno lisemalo, “Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Kama mtu akiharibu hekalu la Mungu, Mungu atmharibu mtu huyo.Kwa maana hekalu la Mungu ni takaatifu, ambalo ndilo ninyi.” (1kor 3:16_17) Tunapokea nguvu, uwezo na mamlaka ya Mungu katika kushirikiana kumtumikia Mungu. Yesu amejitoa nafsi hata kufa ili atukomboe kutoka kwenye mauti. Baada ya kukombolewa tumeingizwa kwenye milki na utawala wa Mungu. Hayo yote ni kwa ajili ya upendo wa Mungu, yatathibitika tukiwa na juhudi katika kutenda mema. Tunatimiza wajibu wetu wa kumtumikia Mungu duniani na baadaye tupate kuurithi uzima wa milele.“Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kutangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu”(1Pet 2:9).“Ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.” (Tit 2:14)Tumeitwa na Mungu ili atufanye kuwa mzao mteule. Ukuhani wa kifalme. Taifa takatifu watu wa milki ya Mungu. Tumeitwa tutoke na tutoe wengine gizani tuingie katika nuru ya kweli yake Yesu Kristo“Ili mwenende kama ilivyo wajibu wenu kwa Mungu, mweenye kuwaita ninyi ili mwingie katika ufalme wake na utukufu wake.” (1 The 2:12)
Viungo vya mwili wa Kristo.
“Kwa kuwa kama katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja. Vivyo hivyo sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika kristo, na viungo kila mmoja kwa mwenzake”(Rum 12: 4 _ 5)
Kutokana na utendaji wa Mungu kama viungo. Kila mmoja ni tofauti na mwingine. Kwa kutumia vipawa vyetu mbalimbali roho Mtakatifu huzitenda kazi hizo zote. Roho humgawia kila mmoja kipawa chake kama apendavyo. Kiungo kimoja kikiumia iwe ni vyote vimeumia. Ndugu yetu wa rohoni akipatwa na shida iwe ni shida yetu sisi sote. Kiungo kimoja kikitukuzwa viungo vingine viungane kwa pamoja kufurahi. Siyo Mungu anapomuinua mwenzetu katika huduma sisi tunachukia. Tufurahi pamoja naye tukimuombea, tukimtia moyo ili Mungu atuinue na sisi tuliobakia. Bila kutengana tunahitaji kuishindania injili kwa pamoja. Tupeane misaada tuhakikishe hakuna mwenzetu anayerudi nyuma au kuanguka dhambini, kwa maana, sisi ni watu washirika lake Yesu Kristo. Tunamfuata Mungu kwa maana sisi ni watoto wake wapendwa. Tukishirikiana sisi watoto wake wapendwa. Tukishirikiana na Yesu anatupenda na kututhamini. Mungu ametutoa dhambini kwa kukubali kumwaga damu yake iwe fidia ya watu wengi ili waokolewe. Yesu anavyotupenda ni wajibu wetu sisi tulio viungo vya Kristo kupendana. Sisi ni viungo tukipendana tutalijenga kanisa imara la Kristo
Umoja wa roho
“Basi pana tofauti za kutenda kazi bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa Ufunuo wa Roho katika kufaidiana Lakini kazi hizi zote huzzitenda Roho huyo mmoja, yeye Yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye. Na kiungo kimoja kikiumiaviungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho.” (1Kor 12:6-7, 11, 26)
Tunatofautiana katika kuitenda kazi ya Mungu vipawa na uwezo wa kila mmoja ni kiungo katika utendaji wa Ki-Mungu. Tukimtumikia Mungu tunaunganishwa na Roho Mtakatifu azitendaye kazi hizo zote tukiunganishwa kuwa kitu kimoja. Tunapewa kila mmoja vipawa kama Roho Mtakatifu apendavyo. Katika kuunganika kwa vipawa hakuna upungufu katika mwili wa Kristo. Tunahitajika kusimama pamoja katika kumtumikia Mungu. Tunatakiwa kuwa na roho moja ili kusababishe mafanikio makubwa katika kushindania Injili. Kuwa na moyo mmoja bila matengano ni mafanikio makubwa katika ulimwengu wa Roho. Mtume Paulo anaeleza muhtasari umoja wa roho unavyopaswa uwe. Jambo kubwa ni unyenyekevu, uvumilivu kuchukuliana katika upendo na kuuhifadhi umoja wa Roha katika kifungo cha imani.
Mambo yafuatayo yanaimarisha umoja wa Roho
·         Bwana mmoja ambaye ni Yesu Kristo.
·         Imani moja.
·         Ubatizo mmoja.
·         Mungu mmoja, muumbaji wa vitu vyote.
·         Kiongozi mmoja.
Hatutahangaika na kitu chochote ikiwa hatutalaumiana wala kulalamikiana. Tukishikana kwa umoja tutaimarishana pia hatutampa Ibilisi nafasi ya utawala kwamaana sisi sote ni viungo kwa vipawa katika mwili wa kristo.

SURA YA KUMI

HUDUMA TANO ZA ROHO MTAKATIFU


Mtu yeyote anapomkubali Yesu awe Bwana na Mwokozi wake amepewa mojawapo.
Naye alitoa wengine kuwa mitume na wengine kuwa manabii, na wengine kuwa wainjilisti, na wengine kuwa wachungaji na walimu” (Efe 4:11).“Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. Pande zote twadhikika bali hatusongwi twaona shaka, bali hatukatitamaa. Twaudhiwa bali hatuachwi, twatupwa chini, bali hatuangamizwi. Siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao, udhihirishwe katika Miili yetu.” (2kor.4:7-10). Huduma hizi zote Mungu kawapa wanadamu wadhaifu. Ila ameweka hazina kubwa kwa nguvu za Roho Mtakatifu. Zipo changamoto nyingi zinazo kabilli huduma hizi lakini Roho Mtakatifu anatutia nguvu. Nguvu inayopatikana katika huduma ni ya Mungu mwenyewe kwa njia ya Roho Mtakatifu. Pia tutambue hakuna huduma isiyo na makwazo na majaribu bali Roho Mtakatikfu anayaondoa ili watu waamini kuwa Mungu yupo. Neno la Mungu linatia nguvu kwamba, “kwahiyo hatulegei, bali japokuwa utu wetu wa Nje unachakaa,lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi iliyo ya muda kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana.” (2kor.4:16-17). Mungu anapotupatia huduma mojawapo kati ya hizo tano ni kwa neema sio kwa nguvu au akili zetu. Kazi ya Mungu tusiifanye kwa ulegevu na woga. Udhaifu wetu wa kibinadamu usitutishe, huu unachakaa na kuharibika, bali tuangalie mambo ya Rohoni ili utu wetu wa ndani ufanywe upya. Tuzihesabu dhiki kwamba sio nzito na hazidumu. Tunapo wahuduumia watu wa Mungu tunangalie utukufu wa Mungu uonekane, maana yake katika kila tendo la huduma Mungu apewe utukufu. Tunapotumika kwa uaminifu utukufu wa Mungu unatuzunguka pamoja na wale tunao wahudumia. Zipo huduma tano ambazo nitazielezea moja moja kama Roho Mtakatifu atakavyo nijalia, ambazo ni Utume, Unabii, Uinjilisti, Uchungaji na Ualimu.
Utume
Huduma hii ilikuwa ikiendelea katika historia ya kanisa. Kwa wakati huu huduma hii inafuatana na ile ya mitume wa kwanza. Huduma hii ni ya kipekee kwasababu inasimamisha msingi wa mafundisho. Mitume wanaanzisha huduma ya Neno la Mungu kwa watu ni waenezaji wa hekima ya Mungu. Mitume wanamsukumo wa kipekee wa kuweka msingi thabiti wa Neno la Mungu .Ni watumishi wenye maono kwa ajili ya kanisa kwa ujumla. Mitume lazima wawe na Roho Mtakatifu maana kuna magumu watakayo kumbana nayo katika huduma yao. Mitume hufanya kazi pamoja na hizi huduma nne zilizobakia. Wao ni wa kiutawala na kiushirika.
Unabii
Manabii wa Agano la kale walikuwa na kazi ya kutoa unabii pamoja na kutangaza. Wanapokea unabii kutoka kwa Mungu kuwatangazia wahusika. Nabii hunena akili na mapenzi ya Mungu kwa ujumbe wa kutabiri, kuongoza hata wakati mwingine kulisahihisha kanisa. Manabii wawe wakomavu na thabiti katika Neno la Mungu na aghalabu ni wenye tabia njema. Manabii ni waonaji, watabiri na wanenaji wa mambo ya Mungu kwa Ufunuo wa maono. Huduma hii ni ya kipekee sana, Mungu ndiye aliyewapatia. Unabii unatokana na matakwa ya Mungu, wasikilizaji wanaupima kwa kupitia Neno la Mungu. Mwenye huduma hii anaweza kuonyeshwa mambo mbalimbali kwa picha au kwa sauti. Wakati mwingine watu wakiwa wanaomba kwa ujumla unabii  unaweza kutokea. Katika kundi la watu  wa Mungu, wapo manabii ambao wana maono kuhusiana na kundi lakini pia kwa kazi ya Mungu.
Uinjilisti
“Kwa kadili ilivyozoeleka Mwinjilisti ni Mtumishi ndani ya kanisa ambaye hubeba dhamana katika kumsaidia Mchungaji wa Usharika.hata hivyo uzoefu unaonyesha kwamba wapo watu wengine ambao kwa kujitolea kwa wito tu pia hufanya kazi ya kuwaongoza washarika na wakristo kumwelekea Mungu. Kwa kufanya hivyo watu hawa huwasaidia wachungaji na watumishi wengine wa kanisa katika kuwaleta kwa Mungu wao. Kuwapo kwa watu wa aina hii kunaifanya dhana ya Mwinjilisti kuwa pana zaidi. Ili kuwajumuisha wao na huduma zao” (Bagandashwa, 2016). Kwa maana hiyo 
Mwinjilisti huduma yake ni kuhubiri injili au habari njema za Yesu Kristo. Anabeba ujumbe wa Injili kwa ajili ya watu. Mwinjilisti ana mzigo maalumu kwa watu waliopotea. Mwinjilisti akiwa amebeba mzigo huo hamfichi mtu anamuambia moja kwa moja juu ya uovu wake. Licha ya watu kuokolewa huduma yao yaweza kuambatana na ishara, miujiza na maajabu ili kuthibitisha Neno la Mungu. Wanjilisti wanapaswa kuwa washarika waaminifu kwa kanisa. Kituo cha wanjilisti ni kwa watu waliopotea, ili watubu waende mbinguni. Kwa ajili ya mzigo kwa waliopotea hatulii hadi watu wametubu na kumpa Yesu maisha. Wanao wajibu mkubwa wa kuwaeleza wengine kuwa na mzigo kwa watu waliopotea na kuwaandaa kwa Uinjilisti. Wainjilisti wanamsukumo wa kuwaelekeza watu wengine kuhusu makosa yao bila kuwaficha, kwa msaada wa Roho Mtakatifu. Mwinjilisti anakemea, anabomoa dhambi na ngome za shetani. Anajenga watu kiroho ili wamfahamu Kristo. Mwinjilisti mwenye huduma hii anatoa mahubiri yenye moto wa Roho Mtakatifu, na watu wanachomwa mioyo na kuamua kutubu mbele za Mungu.
Uchungaji
Mchungaji ni cheo cha Mchunga kondoo. Mchungaji ameitwa ili alishe na kutunza kundi la watu wa Mungu. Mchungaji anahitaji eneo pana la kutolea huduma. Mchungaji ana uwezo wa kulisha kundi la Mungu kwa Neno la Mungu. “Mchungaji ni mtu aliye andaliwa maalum kwa kazi hiyo, akawekwa wakfu na akaajikriwa kuitenda kazi hiyo” (Bagandashwa 2016).
Mtu mwenye huduma hii ana msukumo toka ndani wa kushauri, kupatanisha,kukusanya na kulinda kundi lililopo lisitawanyike. Anafahamu kuwa kundi likitawanyika ataulizwa. Lazima kubeba gharama zinazojitokeza kwa ajili ya kundi la watu wa Mungu. Mchungaji ni mtu ambaye hatakiwi kuwa na lawana. Ifahamike kuwa wapo wachungaji wengine wanaoisaidia, na wengine wanaendelea kuitwa na Mungu. Wenye huduma hii wawe wamekomaa katika Neno la Mungu kwa njia ya maombi.
Mtu naatuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo na mawakilli wa siri za Mungu. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu.” (1kor 4:1-2) wenye huduma hii wanatunza siri za Mungu. Uaminifu unatakiwa uwe sehemu ya maisha yao. Na watu watambue kabisa kwamba huyu ni mtunzaji wa siri za Mungu na za watu wa Mungu. Ni jambo muhimu sana kwa mtumishi mwenye huduma hii kuwa mwaminifu kwa Mungu na kundi analolichunga. Tuyaone maandiko haya yanavyosema kwamba; “Kwasababu hiyo, kwakuwa tunahuduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei. Lakini tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya Neno la Mungu na uongo, bali kwa kuidhihiriisiha iliiyo kweli  twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za Mungu”(2kor.4:1-2). Lazima kuwa na uhakika kwamba Mungu katika Roho Mtakatifu ndiye aliyewaweka Wachungaji katika huduma. Kwa huruma na rehema Mungu anapenda kuwatumia, wanapaswa wasiwe walegevu katika kutimiza wajibu wao mbele za Mungu. Ni muhimu kukataa mambo ya aibu kwasababu yatalifanya Jina la Mungu litukanwe. Uongo unaoletwa na tamaa katika kundi hili usiwepo ili kuepuka kulichanganya Neno la Mungu na uongo. Kuwa wenye haki kwa wanao wachunga na mbele za Mungu. Kutenda haki sio jambo la hiyari bali ni lazima. Dhamiri au nafsi za watu zikifanyiwa haki au udhalimu zinashtaki na kushuhudia mbele za Mungu. Ni kundi linalotakiwa lifanye kazi ya Mungu kwa umakini mkubwa.
Yesu alimwuliza Petro mara tatu Je Simoni wa Yohana wanipenda kuliko hawa? Akajibu wewe wajua kwamba nakupenda. Yesu akamwambia Petro chunga kondoo zangu. Wajibu wa huduma ya Kichungaji ni kulisha kundi kwa Neno la Mungu ili liimarike, liongezeke na kustawi. Kuchunga ni kuhakikisha kundi halisambaratiki na halipotei bali linaendelea kuwepo.
Hebu tuone kidogo ushauri wa Mtume Paulo kwa Timotheo akisema, “Uwakumbushe mambo hayo ukiwaonya machoni pa Mungu, wasiwe na mashindano ya maneno ambayo hayana faida, bali kuwaharibu wasikiao. Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliawa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari ukitumia kwa halali Neno la kweli. Jiepushe na maneno ya siyo na maana, ambayo siyo ya dini, kwakuwa wataendelea zaidi katika maovu.”(2Tim. 2:14-16) Mchungaji akiongozwa na Roho Mtakatifu ataonya na kuwakumbusha watu wadumu katika kumtegemea na kumtumaini Mungu. Wapo watu wanaopenda mashindano na mabishano ambayo katika misingi ya Imani hayana faida. Mchungaji hapaswi kuwa na tabia hiyo bali awasaidie watu hao wasiingie kwenye mshindano. Mchungaji kwa nguvu za Roho Mtakatifu ni mtenda kazi pamoja na Mungu, hakuna sababu ya kuona aibu. Maswali na mashindano huzaa magomvi, mwenye huduma ya kichungaji asiwe mgomvi, bali awe mwanana kwa watu wote. Awezaye kulichukulia kundi katika mafundisho. Ufuatao ni ushauri wa mtume Paulo kwa watu wenye huduma hii, “Lihubiri Neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usio kufaa, karipia,kemea na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. Bali wewe uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya Injili, timiza huduma yako.”(2Tim.4:2,5). Kuna wakati mgumu Roho Mtakatifu anahimiza kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu, hakuna udhuru ni kwenda kama Roho Mtakatifu anavyosukuma. Ili mradi Roho Mtakatifu amemsukuma Mchungaji kukaripia, kukemea na kuonya hata wakatae unabaki kuwa ujumbe wa Mungu. Mchungaji awe na kiasi anayejua kuvumilia mabaya hata kama ameumizwa. Mchungaji analo sharti la kufanya kazi ya mhubiri wa Injili mpaka kufa.
Ualimu
Huduma ya mwalimu wa Neno la Mungu ni muhimu kwa ajili ya afya na ustawi wa kundi . Kanisa lisilo na walimu haliwezi kuimarika wala kukua. Mafundisho ni muhimu maana tunazama ndani kabisa katika Neno la Mungu. Mwalimu anastawisha kweli zenye thamani ndani ya maandiko matakatifu. Anahangaika bila kutulia kutafuta chakula cha kundi liimarike. Mwalimu anapata Ufunuo wa rohoni kwa ajili ya kufahamu mahitaji ya kundi analolihudumia. Baada ya mwinjilisti kufyeka msitu na kuwaleta watu kwa kristo walimu wanawafundisha na kuwajenga. Mtu aliyekosa huduma ya mwalimu kwa kufundishwa ni wepesi wa kuanguka maana katika wokovu hana mizizi ya kutosha. Katika udongo mzuri anapanda na kunyweshea maji ya kukuza mbegu. maji yakuzayo ambayo ni Neno la Mungu.
 Kwahiyo, Huduma hizi zote tano zinajenga mwili wa Kristo. Watu waliojaliwa kuwa nazo ni viungo katika mwili wa kristo. Sisi tulio viungo vya kristo tunapaswa kuhudumiana kwa huduma hizo tano kila mmoja kwa mwenzake.

SURA YA KUMI NA MOJA

KARAMA TISA ZA ROHO MTAKATIFU


Tukitaja karama tunamaanisha kuwa ni kipawa ambacho Roho Mtakatifu anagawa kama apendavyo ili utendaji wa kiroho katika mwili wa Kristo ufanyike, Kama Neno la Mungu linavyosema“Maana mtu mmoja kwa Roho apewa Neno la hekima na mwengine Neno la Maarifa, apendavyo Roho yeye Yule. Mwingine imani katika Roho yeye Yule, na mwingine karama za kuponya katika Roho Yule mmoja na mwingine matendo ya miujiza, na mwingine Unabii, na mwingine kupambanua Roho, mwingine aina za Lugha na mwingine tafsiri za Lugha.” (1Kor 12:8-10)
Kila mmoja anapewa karama kama Roho Mtakatifu apendavyo. Karama ambazo nimefunuliwa ili tujifunze huzitenda huyo Roho Mtakatifu mmoja peke yake.karama hizo ni hizi zifuatazo
Neno la hekima
Karama hii inahusika katika kuhuisha, kuweka nuru au kugusisha Ufunuo wa Ki-Mungu ndani ya maisha yetu. Ni mguso maalum ambao Roho Mtakatifu ameutoa. Katika karama hii Roho Mtakatifu hutoa maono ya ndani na ufahamu wa jinsi ya kuendelea katika hali fulani.Wakati watu wanahitaji kutenda jambo katika kumtumikia Mungu wapo watu wanaoshauri ili kundi hilo lisije likaingia kwenye shida. Yesu katika huduma yake alikuwa na karama hii. Kama tunavyosoma katika Neno la Mungu
Basi utuambie, waonaje? Ni halali kumpa kaisari kodi ama sivyo? Lakini Yesu akaufahamu uovu wao akasema, mbona mnanijaribu. Naowakamletea dinari. Akawaambia ni ya nani sanamu hii, na anuani hii? Wakamwambia ni kaisari. Akawaambia mlipeni kaisari yaliyo ya kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu”
(Mt 22:17-22).
Kwa karama ya Neno la hekima Yesu aligundua mtego wa mashtaka aliotegewa. Hekima namna hii ni muhimu katika kanisa. Bila kuwa na watu wenye karama ya Neno la hekima tunaweza kuteswa tukadhani tunateswa kwa ajili ya kristo kumbe tumekosa hekima toka kwa Mungu.
Vijana Fulani walikwenda kuhubiri mahali Injili kwa watu wasio wakristo. Walijipanga bila kuchukua kibali serekalini. Walidhani watafanikiwa. Walisambaratishwa kwa kupigwa kwa mawe. Walifunguliwa mashtaka wamevunja sheria ya nchi. Walifungwa wakidhani wanateseka kwaajili ya Kristo kumbe ni ujinga wao. Wangefuata utaratibu wa kuomba kibali cha Mkutano hayo yasinge wapata. Wahubiri tujitahidi kuwa na hekima tusidharau taratibu. Karama hii ya Neno la hekima inafanya kazi ndani ya watu wenye huduma ya unabii na uchungaji.

Neno la maarifa
Watu wenye karama hii wanapata Ufunuo wa Ki-Mungu kuhusu kiwango Fulani cha elimu ya Mungu. Ni mambo muhimu ambayo yanaonyesha kiroho mambo yasiyoonekana kwa macho ya wanadamu. Ni taarifa ya mambo ya kina ambayo hayawezekani kwa wanadamu. Uthibitisho wa Neno la maarifa ni mguso wa moja kwa moja au uhuisho wa akili ya mpokeaji kwa akili ya Mungu ajuaye yote (Yn. 4:18). Ni hali inayoonekana kiroho lakini kimwili haiwezekani.
Katika Ufunuo huu hali ya mtu mwenye shida inahamia kwa mtu mwenye Neno la maarifa. Taabu na maumivu ya mtu mwenye shida yanahamia kwake. Inakuwa hivi maumivu au matatizo hayo hayakuumizi na yanakuja ghafla. Ukiona hivyo ujue kuna mtu mwenye hiyo hali. Ndiyo maana wakati mwingine umesikia au utasikia watumishi wakisema kuna mwenye maumivu kichwani, mgongoni, kifuani nk. hali ile anayoitaja anaihisi yeye. Huduma zinazoambatana na karama hii ni uinjilisti, ualimu na utume
Imani
“Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao akasema; wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung’oa nanga huko Krete na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa naawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwamaana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea ila Malekebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo Malaika wa Mungu Yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami, akaniambia usiogope, Paulo huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. Basi, Wanaume changamkeni, kwasababu namwamini Mungu, yakwamba yatakuwa vilevile kama nilivyoambiwa.”Mdo 27:21-25
Hii ni karama itolewayo na Roho Mtakatifu kwenda kwa muumini kwa ajili ya hali zisizowezekana. Inatumika kwa uweza wa Mungu siyo uweza wa Kibinadamu. Imani ni ule uhakika wa kutimiza majukumu maalimu na kupambana na hali zinazotuzidi uwezo. Kazi ya karama ya imani ni kutuhifadhi katika hali ya hatari. Unabii unaweza kutolewa kutokana na lile Mungu analotaka watu walifanye au wasilifanye.
Karama hii inaambatana na huduma ya unabii na uchungaji
Uponyaji
Karama za uponyaji ni uwezo wa Ki-Mungu wa kuhudumia uponyaji wa Kimwili na madhaifu. Tukisema karama za uponyaji ni wingi tukimaanisha kwamba ni uwezo wa uponyaji wa kimwili, kiroho kiakili hata kisaikolojia. Yesu Kristo anasema,
“Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio kwa Jina langu watatoa pepo, watasema kwa lugha mpya watashika nyoka, hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa. Wataweka mikono yao juu ya wagonjwa nao watapata afya” (Mk 16:17-18).Kwa ishara ya kuweka mikono juu wa wagonjwa wanapokea uzima. Ni nguvu ya Mungu ndiyo inayofanya kazi siyo ujuzi wa muombaji. Karama hii inafanya kazi pamoja na mitume wainjilisti na walimu.
Matendo ya miujiza
Miujiza ni jambo la Ki-Mungu. Karama hii humhitaji Mungu atende kazi kwa kupitia watu fulani. Ni kutenda yasiyowezekana kwa akili za wanadamu.“Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda, mara kiwi kikamuangukia na giza, akazungukazunguka na kumtafuta mtu wakumshika mkono na kmwongoza” (Mdo 13:11)Matendo ya miujiza yanathibitisha Neno la Mungu.
Karama hii inafuatana na wainjilisti, mitume na walimu
Unabii
Ni kuruhusiwa kunena chini ya uongozi wa moja kwa moja kutoka kwa Roho Mtakatifu. Kimsingi waliojaliwa karama hii wanatangaza kwa hali ya kuinuliwa katika Ufunuo wa kuhuishwa na akili ya Mungu. “Mtu huyu alikuwa na mabinti wane mabikira, waliokuwa wakitabiri,Basi tulipokuwa tukikaa huko siku nyingi, Nabii mmoja jina lake Agabo akashuka kutoka Uyahudi. Alipotufikia aliutwaa mshipi wa Paulo, akajifunga miguu na mikono akasema, Roho Mtakattifu asema hivi, Ndivyo Wayahudi wa Yerusalemu watakavyo mfunga mtu mwenye mshipi huu, nao watamtia katika mikono ya watu wa mataifa.”(Mdo.21:9-11)
Karama hii inafanya kazi ndani ya manabii.
Kupambanua roho
Ni uwezo wa Ki-Mungu wa kutambua chanzo cha kiroho. Uwezo huo unafuatana na Nenohisia au tendo ndani ya mtu au kundi la watu au nguvu za giza. Karama hii inathibitika kwa wote waliojazwa Roho Mtakatifu“Lakini Petro akamwambia, Fedha yako na ipotelee mbali pamoja nawe, kwakuwa umedhania yakuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali. Huna fungu wala huna sehemu katika jambo hili kwakuwa moyo wako si mnyoofu mbele za Mungu.”(Mdo 8:20-21). Zipo aina nyingi za maroho tusipokuwa na watu wenye uwezo wa kupambanua tutashindwa na Ibilisi maana atatutegea.
Karama hii hufanya kazi pamoja na hizi hudma zote tano.
Kunena kwa lugha
Yapo Maneno ya Mungu yanayozungumzia kuhusu kunena kwa Lugha kama ifuatavyo: “Petro alivyokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote walio lisikia lile Neno na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja na Petro, kwasababu mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha na kumuadhimisha Mungu.”(Mdo 10:45-46). Bali yeye ahutubuye asema na watu maneno ya kuwajenga, na kuwafariji na kuwatia moyo. Yeye anenaye kwa lugha hujijenga nafsi yake bali ahutubuye hulijenga kanisa.”(1Kor.14:3-4)
Kunena kwa lugha ni uwezo wa Ki-Mungu wa kuwasiliana na Mungu kwa lugha zaidi ya moja sliyoizoea. Karama hii inaweza kugusisha lugha za wanadamu au lugha za malaika. Karama hii hupatikana kwa waamini wote. Hii ni karama pekee inayotusaidia katika kujijenga kiroho. Ukinena kwa lugha mpya unaongeza chaji za kiroho ndani yako. Ni msukumo ambao unatoka ndani yetu tuliookoka ili kuteketeza na kuanguasha ngome na utawala wa ibilisi.
Karama hii inahusika na huduma zote tano.
Tafsiri za lugha
Karama hii pia ni ya Ki-Mungu. Ufunuo wake umekuja wenyewe. Inahusika katika kutafsiri tamko linalokuja kwa lugha mpya kwa lugha inayoeleweka kwa watu waliopo. Huku kutafsiri lugha hakuhusiani na lugha za kawaida bali huja moja kwa moja kutoka kwa Mungu“Yamkini ziko sauti za namna nyingi Duniani, wala hakuna moja isiyo namaana. Basi nisipoijua maana ya ile sauti nitakuwa kama mjinga kwake yeye anenaye: naye anenaye atakuwa mjina kwangu. Kwasababu hiyo yeye anenaye kwa Lugha na aombe apewe tafsiri. Maana nikiomba kwa lugha, Roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda.”(1Kor 14:10-11, 13-14)Karama hii inaambatana na manabii.
 Kwahiyo, Kama wewe ni kiungo katika mwili wa kristo na unayo kiu ya kupata karama hizi basi Roho Mtakatifu atatukirimia.Karama hizi zote nilizozifafanua zipo kwa ajili ya kujenga mwili wa kristo

SURA YA KUMI NA MBILI

VIPAWA NANE VYA UTENDAJI KATIKA ROHO MTAKATIFU


Katika utendaji wa huduma na karama nilizokwisha eleza kila mmoja amepewa vipawa vyake. Vipawa mtu anazaliwa na kukua akiwa navyo. Tunaweza kuviita ni vipawa vya umbaji ambavyo havijaboreshwa na Roho Mtakatifu au mafundisho. Watu wengine hata kama hawajamfahamu Yesu Kristo, kuwa ni Bwana na mwokozi wao, wanayomambo ambayo wanafanya. Yanatofautiana kati ya mtu na mtu. Tuvione vipawa hivyo katika Neno la Mungu lisemalo “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbali mbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa Unabii tutoe unabii kwa kadiri ya Imani. Ikiwa huduma yetu; mwenye kufundisha kwake. Mwenye kuonya katika kuonya kwake; mwenye kurehemu, kwa furaha.” (Rum.12:6-8). Uzoefu unaonyesha kwamba vipawa mtu anazaliwa navyo. Vinajitokeza katika kuendelea kukua. Wakatianashangaa anafanya akiona ni kawaida, vinaitwa vipawa vya umbaji. Vipo vipawa ambavyo tunatengenezewa kupitia mafunzo mbalimbali. Hata kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.” (Bagandashwa,2016)Vipawa ambavyo nitavielezea ni kuhudumu, Kufundisha, kuonya, kukarimu, kusimamia, kurehemu na kuimba.
Kipawa cha unabii
Kipawa hiki kinahusika katika kunena chini ya ulaini wa Roho Mtakatifu. Ki-Msingi ni kipawa cha utendaji chini ya utawala wa Roho Mtakatifu. Kina msukumo wa kutangaza akili ya Mungu chini ya uvuvio wa kuhuisha. (1Kor 14:13).Kipawa hiki kazi yake kuwatia moyo waliovunjika moyo na kukatatamaa, waliojeruhiwa na kuumizwa ili wapate nguvu tena.

Kipawa cha kuhudumu

Kipawa hiki kinahusu msukumo wa kutumikia ili kukidhi haja iliyopo. Kwa kawaida watu wenye kipawa hiki ni wasaidizi wenye utayari wa kutumika na kuwajibika. Watu wenye kipawa hiki wakifanya jambo likifanikiwa wanatosheka, wanardidhika na kupata amani. Watu hawa wanakuwa ni wa baraka kwa uongozi kwa ajili ya kazi yao ya kujitolea.
Kipawa cha kufundisha
Ni msukumo wa kutafiti na uwezo wa kuwaelezea watu wengine kweli zinazopatikana katika Neno la Mungu. Ni watu wanaotoa mafunzo ya Neno la Mungu kwa wengine. Ni wasaidizi katika Shule ya Jumapili, Mikutano ya nyumbani na usafi wa kanisa. Kutokana na thamani ya kipawa hiki wanaweza kuingia katika huduma ya ualimu “Basi myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa Elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwakuwa Roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu.(Mdo18:24-25). Apolo alikuwa mtu aliyesoma anayehitaji kujifunza mambo mengi. Alichunguza, alisoma, alisikiliza na kupekua Neno la Mungu akawa hodari wa maandiko. Naye alipata nafasi ya kufundisha.  Kwa wengine kipawa hiki kinaanza na kukua polepole hadi kufikia uhodari na ufundi wa maandiko. Biblia inasema roho yake ilimuaka, maana yake amepata msukumo usio wa kawaida kufundisha Neno la Mungu kwa usahihi. Wenye kipawa hiki wakifunuliwa kuwa watu hawajui, watapata msukumo wa kuwafundisha kutokana mahitaji yao. Kufundisha huku hutokana na msukumo maalumu wa mtu binafsi.

Kipawa cha kuonya

Kuonya ni kusihi, kuusia,kutia nguvu,kufariji na kutuliza. Kumtia mtu moyo ni hali inayotokana na mtu aliyekata tamaa. Mtu mwenye kipawa hiki anauwezo wa kuwakilisha ushauri kwa kutia moyo na kutoa maonyo na maelekezo sahihi kwa watu wengine. Mwenye kipawa hiki anaomzigo kwaajili ya kusaidia watu wengine kuonya ni tendo la kuzaa matunda

Kipawa cha kukarimu

Mkarimu ni mtu mwenye kipawa cha utoaji. Anafurahia kuchangia kwa kutoa fedha au mali kwa ajili ya kazi ya Mungu. Watu wa namna hii wanamsukumo wa kutoa mali zao bila kujali kupungukiwa. Mkarimu siku zote hatapungukiwa bali atakuwa mtu wa baraka nyingi kutoka kwa Mungu“Na Yusufu aliyeitwa na Mitume Barnaba,(maana yake mwana wa faraja), Mlawi, asili yake ni mtu wa Kipro, alikuwa na shamba, akaliuza, akaileta fedha, akaiweka miguuni mwa mitume.”(Mdo 4:36-37)

Kipawa cha kusimamia

Mwenye kipawa hiki anamsukumo wa pekee wa kuongoza wengine kwa kutimiliza mapenzi ya Mungu. Wanauwezo wa kushauri na kuongoza wengine katika kustawisha maeneo mbalimbali ya huduma. Kipawa cha uongozi ni muhimu kwa utendaji wa kazi ya Mungu. Tusome Neno la Mungu lisemalo “NaMungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu miujiza, kasha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano na maongozi, na aina z lugha.” (1kor 12:28) Katika mstari huu wa Biblia lengo hasa ni maneno haya “masaidiano na maongozi” ndiyo yanayoendeana na kipawa cha kusimamia.
Ni budi kipawa hiki kiwepo katika uongozi wa kanisa la mahali pamoja. (Dhehebu). Ni muhimu kwa huduma ya kiuchungaji na kitume (Mdo 2:14). Wanakuwa na mzigo ili mambo yasiharibike.

Kipawa cha kurehemu

Wenye kipawa cha rehema huonekana kuwa na hisia kali ya huruma kwa wale wanaopata matatizo au mateso kutokana na kuumizwa. Huruma yao huwaongoza katika matendo ya huruma, hutia msaada na faraja kwa wahitaji .Chimbuko la rehema ni Mungu wetu“Bwana amejaa huruma na neema. Haoni hasira upesi ni mwingi wa fadhili.(Zab.103:8)“Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. Msihukumu nanyi hamatahukumiwa, msilaumu nanyi hamtalaumiwa achilieni nanyi mtaachiliwa”(Luka 6:36-37);).Sisi  watoto wa Mungu tuliokombolewa tunatakiwa tuwe na rehema. Tuone uchungu mzito wenzetu wakiteseka. “Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.” (Mt 5:7) kwa mujibu wa mahubiri ya Yesu anasema wamebarikiwa watu ambao wanawahurumia watu wengine. Watu wenye kipawa cha kurehemu nao Mungu atawarehemu, sawa sawa na rehema zao. Hebu tusome pamoja Neno hilimaana hukumu haina huruma yake yeye asiyeona huruma. Huruma hujitukuza juu ya hukumu.”(Yak.2:1)

Kipawa cha kuimba

Wenye kipawa hiki wanamsukumo maalumu wa kumsifu na kumtukuza Mungu. Kutoa sifa kwa kuimba kunakigusa kiti cha enzi cha Mungu. Wenye kipawa hiki huchangamsha, huleta uamsho kanisani wakati wote wa makusanyiko. Kuimba ni njia ya kuhubiri ukuu na Mamlaka ya Mungu.
 Kwahiyo, vipawa vyote nane kila mmoja aliyeokoka amepewa baadhi. Maana yake huwezi kuwa navipawa vyote. Ili tuujenge ufalme wa Mungu duniani tumuombe Mungu atusaidie kufufua vipawa vilivyokufa. Hata wewe rafiki yangu ambaye hujampa Yesu maisha, Utakapofanya hivyo na wewe utakirimiwa vipawa. Tuamke ili tuitende kazi ya  Mungu maadamu ni mchana. “Mwimbieni Bwana wimbo mpya. Kwa maana ametenda mambo ya ajabu. Mkono wa kuume wake mwenyewe, mkono wake Mtakatifu umemtendea wokovu. Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote. Mtumikieni Bwana kwa furaha. Njoni mbele zake kwa kuimba.” (98:1,99:1). Mfalme Daudi  anawahimiza watu wote wamwimbie Bwana. Tunaimba kwasababu Mungu ametenda mambo ya ajabu. Tunaaowajibu wakuzipaza sauti zetu mbele za Mungu. Tunapoimba tunatimiza majukumu yetu ya kumtumikia Mungu. Kuimba ni kuburudisha nafsi zetu na za wengine. Kuimba ni sehemu ya maisha ya mkristo. Zipo sababu kadhaa zinazotufanya tuimbe wimbo katika kipawa. Kuimba ni sehemu moiawapo katika Ibada.Mungu anazipenda sifa tunazompazia kwa sauti zetu. Tunapoimba tunammgusa Mungu. Tunajitahidi kumpendeza Mungu tunapoimba. Tunammshuuhudia Yesu Kristo kwaajili ya Matendo yake makuu. Kuimba sio hiyari ni lazima kwa watu wenye kipawa hicho. Nyimbo zinaushushusha uwepo wa Mungu na kuleta utukufu wa Mungu.




























AHSANTE SANA KWA KUSOMA KITABU HIKI.
USIACHE KUKIOMBEA TAYARI KIPO KINAKAMILIKA TAYARI KWA KUWEKWA DUKANI. Usikose Kupata kitabu kizima chenye sura zote Kumi na Tatu. Utajifunza Mengi katika hayo yote utamtukuza Mungu


Mungu Akubariki!!

























Hakuna maoni:

Chapisha Maoni